SHIRIKA la Grumeti Fund katika kuendelea kugusa maisha ya Wananchi hasa waishio pembezoni mwa Hifadhi ya taifa ya Serengeti, imeendesha mafunzo ya ujasiriamali ya utengenezaji wa batiki kwa wanakijiji cha Park Nyigoti mafunzo ambayo yanalenga kuondoa utegemezi wa shughuli za uwindaji na ukataji wa mkaa katika Hifadhi hiyo.
Akizungumza wakati wa mafunzo hayo, Afisa Mradi wa Ustawishaji wa Biashara kutoka Grumeti Fund Ndg. Nelson Petro akifafanua dhamira kuu ya mafunzo hayo amesema ni kutoa fursa mbadala za kiuchumi kwa wananchi itakayosaidia kuondoa utegemezi wa hifadhi badala yake kufanya shughuli nyingine zo za kuwaingizia kipato.
"Tunatambua umuhimu wa jamii zinazoishi jirani na hifadhi kushiriki kikamilifu katika uhifadhi. Njia bora na kufanya hivyo ni kuhakikisha wanakuwa na vyanzo vya uhakika vya mapato vinavyowapunguzia utegemezi wa moja kwa moja wa rasilimali za hifadhi kama vile kuni, uwindaji haramu, au kilimo kisicho endelevu ndio sababu kubwa ya Grumeti kuendesha mafunzo haya" alisema Nelson
Mafunzo haya yameundwa kwa kuzingatia mbinu za kisasa za utengenezaji wa batiki, kuanzia hatua za awali za uandaaji wa malighafi, uchoraji, uchapaji, hadi hatua za kumalizia bidhaa. Washiriki wanajifunza jinsi ya kutumia rangi zisizodhuru mazingira na mbinu za ubunifu zitakazowafanya batiki zao kuwa na mvuto sokoni.
Naye Bi. Chausiku Elias ambaye ni mshiki wa mafunzo haya ameeleza jinsi mafunzo haya yatakavyobadilisha maisha yake ambapo wamesema
"Nimekuwa nikitegemea sana kuchoma mkaa ambao unaharibu sana mazingira, Sasa nimepata ujuzi mpya ambao nitaweza kuutumia kujipatia kipato muda wote. Ninaamini batiki zitafungua milango ya fursa kwangu na kwa wanawake wenzangu kijijini." Alisema
Kwa upande wa wanaume, Bw. Jumapili Sontome amesema, "Tunashukuru sana Grumeti Fund kwa kutupa ujuzi huu. Sisi kama kama wanaume mara nyingi siku hizi tunaachwa nyuma, ujuzi wa batiki unatupa uwezo wa kujiajiri na hata kuajiri wengine. Hii itapunguza changamoto za kiuchumi tunazokabiliana nazo."
Grumeti Fund imekuwa ikifanya kazi kwa karibu na serikali za mitaa na wadau wengine wa maendeleo ili kuhakikisha programu zake zinafanikiwa na kuwa na athari chanya ya kudumu. Mafunzo haya ya batiki ni sehemu ya mkakati mpana wa shirika la Grumeti Fund kuwekeza katika elimu, afya, na uwezeshaji wa kiuchumi kwa jamii zinazopakana na hifadhi, huku likisisitiza umuhimu wa uhifadhi wa wanyamapori na mazingira.
Kukamilika kwa mafunzo haya kutaambatana na msaada wa kwanza wa masoko ili kuhakikisha washiriki wanaweza kuanza shughuli zao mara moja na kujipatia kipato. Hatua hii inaashiria hatua muhimu kuelekea kujenga jamii imara kiuchumi na rafiki wa mazingira.
31603 Stendi Kuu | Serengeti
Anuani ya Posta: 176 Mugumu Serengeti
Simu ya mezani: 0282985686
Simu: 0782677763
Barua pepe: ded@serengetidc.go.tz
Hakimiliki © 2018 Halmashauri ya Wilaya ya Serengeti